Kigoma Online News

FURNITURE

KALIHAMWE STATIONARY

KALIHAMWE STATIONARY

Jul 31, 2015

KAFULILA AWAFUNGA MIDOMO ACT



Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kusini David Kafulila amewajibu  baadhi ya wakazi wa jimbo hilo waliokuwa wakidai mbunge huyo atahamia chama cha ACT kwa kuchukua fomu ya kuwania tena nafasi hiyo  kupitia chama cha NCCR Mageuzi.

Akizungumza baada ya kuchukua fomu ya ubunge hapo jana, Kafulila alisema kuwa yeye bado ni mwanachama wa NCCR Mageuzi na ataendelea kuwatumia wananchi kupitia chama hicho ambacho kwake anakiona ndio bora.
Kafulila akiwapungia mkono wakazi wa Nguruka waliofurika kwenye uwanja wa Shule ya Msingi Nguruka kushuhudia tukio la kuchukua fomu kuwania tena nafasi hiyo.

“Nadhani kitendo nilichofanya leo cha kuchukua fomu kitawafanya msiendelee kuamini minong’ono ya watu pia kwa kauli yangu mwenyewe nasema siwezi kuhamia chama cha ACT-Wazalendo” alisisitiza.

Aidha Kafulila ambaye aliwasili jimboni kwake Jana na kupata mapokezi makubwa kutoka Kwa wakazi wa Nguruka na baadaye kukabidhiwa fomu ya ubunge na wazee wa kata ya Nguruka wakiongozwa na Sheikh Rajabu Kagina, baada ya kulipia kiasi cha shilingi elfu 50.
Kafulila akionyesha fomu ya kugombea ubunge jimbo la Kigoma Kusini kupitia NCCR Mageuzi, baada ya kukabidhiwa na wazee wa Kata ya Nguruka wakiongozwa na Sheikh Rajabu Kazina.

Baada ya kukabidhiwa fomu hiyo Kafulila aliwashukuru wananchi wa Jimbo la Kigoma Kusini kwa ushirikiano waliompa katika kuleta maendeleo na kisha kuelezea mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka mitano yeye akiwa Mbunge.

Alisema kuwa katika kipindi chake kinachomalizika amejitahidi kwa asilimia kubwa kuleta mabadiliko jimboni ambapo ameweza kutatua baadhi ya kero za wananchi ikiwemo kusomesha watoto 200 ambao wazazi wao hawana uwezo wa kugharamia masomo.

Alieleza mafanikio mengine kuwa ni pamoja na kununua vifaa vya maabara kwa shule za kata 17 zilizoko jimboni humo, vitanda na magodoro kwa ajili kina mama kujifungulia katika kituo cha afya Nguruka na kumaliza tatizo la kina mama kulala wawili wawili kwenye kitanda kimoja.

Aidha alieleza kuwa amesaidia kuchimba visima vya maji katika baadhi ya vijiji ikiwemo Kijiji cha Mtego wa Noti na kijiji cha Muganza pamoja na kuwezesha wakazi wa vijiji hivyo na vijiji Jirani kupata mawasiliano ya simu na barabara.

Nao baadhi ya wakazi wa Kata ya Nguruka wakiwemo Bernard Banama, Mathayo James na Mariam Sigele, walipoulizwa walisema yote yaliyoelezwa na Mbunge wao ni sahihi kuwa ameleta tofauti ukilinganisha na wabunge waliotangulia na kwamba wao wataendelea kumuunga mkono na kuahidi kumchagua tena mwezi Octoba.

Mwisho.