Kigoma Online News

FURNITURE

KALIHAMWE STATIONARY

KALIHAMWE STATIONARY

Jul 25, 2015

NHIF YATOA KADI ZA BIMA YA AFYA KWA WANAHABARI KIGOMA



MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umekabidhi vitambulisho vya uanachama wa mfuko huo kwa Waandishi wa Habari Mkoa wa Kigoma waliojiunga na mfuko huo ambao huwanufaisha wanachama wake kupata huduma za matibabu bure katika hospitali na zahanati ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akikabidhi vitambulisho hivyo hapo jana katika Ofisi za Chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Kigoma (KGPC), Meneja wa NHIF, mkoani hapa, Elias Odhiambo, sambamba na kuwapongeza wanahabari hao kwa hatua waliochukua pia aliwataka kuwa mabarozi wazuri kwa vyama vingine vya wanahabari.
Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Mkoa wa Kigoma, Elias Odhiambo, kushoto akimkabidhi kitambulisho cha uanachama wa mfuko huo, mmoja wa Waandishi wa Habari Mkoa wa Kigoma ambaye pia ni Mwenyekiti wa KGPC, Deo Nsokolo.

Alisema kuwa, KGPC inaonyesha mfano kwa vyama vingine ambavyo bado havijajiunga pia ukomavu katika kujari afya zao na matumizi ya pesa, na ni moja ya Vyama  vichache ambavyo wanachama wake wamejiunga na mfuko huo, hivyo KGPC inakuwa mfano kwa vyama ambavyo bado havijajiunga.

“Hapa nchi kuna vyama vingi vya wanahabari katika kila mkoa ila ni vyama vichache ambavyo vimejiunga na NHIF, hivyo tumaini letu ni kwamba mtawahamasisha hata wengine kujiunga katika mfuko huu” alisema Odhiambo.

Aidha Odhiambo aliongeza kuwa, NHIF ina manufaa makubwa kwa mtu anaejiunga na mfuko kwani huchangia mara moja tu na baada ya kuchangia atatibiwa bure popote pale  nchini katika kipindi cha mwaka mzima.

Hata hivyo aliwataka wanahabari kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu faida za mfuko huo ambazo kimsingi zinampa mwananchi fursa ya kutotumia pesa wakati anapougua kwani akiwa na kadi na NHIF anatibiwa bure.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa (KGPC), Deogratius Nsokolo, alisema kuwa mfuko huo ni muhimu sana kwa waandishi wa habari hasa ukizingatia kuwa  hufanya kazi katika mazingira magumu na hatarishi.

“Mara nyingi huwa tunasafiri hapa na pale katika shughuli yetu ya habari na magonjwa kwa binadamu huwa hayatoi taarifa, huja tu muda usio tarajia, hivyo kama unakadi ya NHIF, una fursa ya kupata matibabu popote pale utakapopata matatizo ya magonjwa” alisema Nsokolo.

Wanahabari waliojiunga na mfuko huo na kukabidhiwa kadi zao ni pamoja na Deogratius Nsokoro (ITV),Adela Madyane (Kigoma Yetu),  Fadhir Abdalah (Habari Leo), Mwajabu Kigaza (Majira), Magreth Magoso (Jambo Leo).