Kigoma Online News

FURNITURE

KALIHAMWE STATIONARY

KALIHAMWE STATIONARY

Jul 11, 2015

WANASIASA WATAKIWA KUTOKUWA CHANZO CHA VURUGU WAKATI WA KAMPENI NA UCHAGUZI



WANASIASA wa vyama vyote nchini ambao ndio wadau wakubwa wa uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Octoba mwaka huu wametakiwa kutokuwa chanzo cha vurugu na migawanyiko ya aina yoyote ambayo inaweza kuhatarisha amani ya nchi.

Kauli hiyo ilitolewa hapo jana na Umoja wa Maaskofu na Wachungaji Mkoani Kigoma katika Ufunguzi wa mkutano wa Injili unaoendelea katika viwanja vya Community Center katika Manispaa ya kigoma – Ujiji.

Akisoma risala kwa niaba ya Maasko na Wachungaji mkoani hapa, Mchungaji wa Kanisa la Pentecote Assembless Of God Tanzania (PAGT-Katubuka), Michael Kulwa, alisema kuwa, wanasiasa hawanabudi kujilinda na kauli, lugha na matamshi ili kuufanya kampeni za uchaguzi na uchaguzi wenyewe kukamilika kwa amani na utulivu.

Kulwa alisema kuwa, kitendo cha wanasiasa kutokulinda kauli zao kunaweza kusababisha madhara makubwa na hata umwagikaji wa damu usio na sababu hivyo wote kwa pamoja wanatakiwa kukumbuka amani ya Tanzania inatakiwa kulindwa kila wanapokuwa Jukwaani kunadi sera zao.

“Ushauri wetu sisi Maaskofu na Wachungaji Mkoani Kigoma ni wanasiasa kufuata sheria na taratibu zilizowekwa ili kuilinda amani ya nchi yetu,” alisema Kulwa.


Aidha Kulwa alisema kuwa, wao kama Watumishi wa Mungu wanaahidi kuendelea kushirikiana na serikali pamoja na vyombo vyake vya dola katika kuhakikisha ambani ya nchi inaendelea kutawala kwa muda wote wa kampeni hadi uchaguzi na baada ya uchaguzi.

“Pia tutaendela kuwanyooshea vidole waovu kila iitwapo leo. Kwa kuonya na kukemea maovu ya kila aina ikiwemo rushwa, wizi wa mali za umma, uzembe kazini na ukiukwaji wa sheria unaofanywa kwa makusudi” alisisitiza.


Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Kanali Mstaafu Issa Machibya, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mkutano huo, aliwataka wananchi kutokukubaliana na wanasiasa watakaotaka kuwagawa kwa misingi ya udini na ukabila na wala wasikubali kutumiwa kwa namna yoyote ile kuleta vurugu.

Machibya aliema kuwa, ni jukumu la kila mmoja kulinda amani ya nchi sasa kama wananchi watakubali kutumiwa kuleta vurugu basi watakuwa wanaiingiza nchi yetu katika machafuko ambayo yanaweza kupelekea umwagaji wa damu.


“Nitoe angalizo kwa wananchi wote kuhusu viongozi wanaotafuta madaraka kwa kutumia rushwa, hebu tujiulize, huyu atakayepata madaraka kwa kutoa rushwa, je ataweza kukemea vitendo vya rushwa na ufisadi pindi atakapokuwa madarakani? Jibu ni hapana” aliongeza Machibya.