Kigoma Online News

FURNITURE

KALIHAMWE STATIONARY

KALIHAMWE STATIONARY

Jul 2, 2015

WAZEE KIGOMA WAMCHUKULIA FOMU YA UBUNGE DR. YARED FUBUSA



WAZEE wa Kijiji cha Kiganza Kata ya Mwandiga katika Jimbo la Kigoma Kaskazini lililoko Wilaya ya Kigoma Vijiji wamemchukulia fomu ya kugombea Ubunge wa Jimbo hilo Mjumbe wa Kuchaguliwa Kamati Kuu Taifa CHADEMA, Dkt. Yared Fubusa kupitia Chama hicho baada ya kuona anafaa kuongoza jimbo lao kutokana na kukerwa na tabia za Wabunge waliopita.

Akizungumza kwaniaba ya Wazee wenzake hapo jana wakati wakimkabidhi fomu hiyo, Mwenyekiti wa Wazee Wilaya ya Kigoma (CHADEMA) Mzee Yasini Athumani (Mapigosaba) alisema kuwa, Kiu yao kubwa ni kupata mbunge ambaye atakaa na wananchi na kufahamu matatizo yao badala ya kwenda kuishi Dar es Salaam baada ya kuchaguliwa.
Mwenyekiti wa Wazee Wilaya ya Kigoma, Mzee Yasini Athumani (Mapigosaba) akimkabidhi fomu Dkt. Yaredi Fubusa

Alisema kuwa, baada ya Zitto Kabwe kushindwa kulitumikia Jimbo lake sambamba na kufukuzwa katika chama walikaa wao kama wazee wa Kijiji cha Kiganza na kutafuta ni nani anayeweza kuwa Mbunge wao ambaye ataweka mbele maslahi ya Jimbo.

“Tuliona Dkt Yared anatufaa sana kulingana na tabia aliyoionyesha kwa wananchi wa Kiganza sambamba na mchango mkubwa wa Elimu anaoutoa katika Jimbo vitu ambavyo havikufanywa na Wabunge waliopita” Alisema Athumani.
Mjumbe wa Kuchaguliwa Kamati Kuu Taifa CHADEMA, Dkt Yaredi Fubusa akizungumza na wananchi baada ya kukabidhiwa fomu na wazee wa Jimbo la Kigoma Kaskazini

Mzee Athumani alisema, Licha ya kuwa Fubusa ni Mjumbe wa Kamati Kuu CHADEMA  Taifa hilo wao hawakuangalia walichoangalia ni elimu aliyonayo na mali alizo nazo lakini hakupenda kuishi kwenye mikoa iliyoendelea bali anaishi na wanakijiji wenzake huku akitumia Elimu yake na mali zake kuwasaidia wananchi.

“Moyo wake wa Upendo kwa watu wa kijiji chake unatufanya tuamini ndie anayeweza kutuwakilisha kwani kama amejenga shule mbalimbali katika jimbo hili akiwa ni mwananchi wa kawaida basi anaweza kufanya makubwa akiwa Mbunge” aliongeza Mzee Athumani.

Kwa mujibu wa Mzee Athumani, walichukua Fomu hiyo kwa gharama ya shilingi 27000/= na kuamini kuwa kumchukulia fomu itakuwa faida kwao kwani watakuwa na uwezo wa kumbana endapo itatokea akikosea.

“Tunamuomba Yaredi atutoe aibu Jimbo la Kigoma Kaskazini kuwa nyuma kimaendeleo na asiwe kama wale Wabunge waliopita ambao wakifika Bungeni kazi yao ni kuongelea BUZWAGI, EPA na ESCROW na kusahau kulizungumzia jimbo lao” alisisitiza Mzee Athumani.

Kwa upande wake Mjumbe wa Kuchaguliwa  Kamati Kuu CHADEMA Taifa, Dkt Yaredi Fubusa, aliwashukuru wazee hao kwa kuona umuhimu wake kwa jamii na kumuamini na kumpa dhamana ya kuwatumikia kama Mbunge.

Fubusa alisema, kitendo cha wazee kumchukulia Fomu kimempa hamasa ya kuanza kufikilia ni wapi ataanzia katika kuwatetea wananchi baada ya kuchaguliwa na kuwaahidi kutokuwaangusha kama atapitishwa na CHADEMA kugombea Ubunge wa Jimbo hilo.

“Ni bora ningechukua fomu mwenyewe kidogo ningejitetea pindi nikikosea  lakini kama wamenichukulia wao basi hapo sitakuwa na cha kujitetea ila nachowaahidi nipo kwaajiri ya kuwatumikia kama walivyoniamini” alisema Fubusa.

Wakati huohuo, waliotangza nia ya kugombea nafasi ya Ubunge katika majimbo mbalimbali mkoani Kigoma wameendelea kurejesha fomu hizo na kusubiri iwapo watapewa nafasi na CHADEMA ya kugombea nafasi ya ubunge katika Uchaguzi ujao.

Basilius Budida ambaye alichukua fomu ya kuwania nafasi ya kugombea Ubunge katika Jimbo la Manyovu alirejesha fomu hiyo hapo jana na kuwataka wananchi kumuunga mkono endapo atapitishwa na chama chake.

“Uchaguzi wa mwaka 2010 sikupata ushindi baada ya kufanyika kwa ufedhuri katika kura zilizopigwa na kutoa nafasi kwa mgombea wa CCM ila mwaka huu nawaomba wananchi kujitokeza kwa wingi ili kuwaonyesha walioiba kula mwaka jana kuwa mwaka huu ni wa Upinzaji kuchukua madaraka” alisema Budida.