Kigoma Online News

FURNITURE

KALIHAMWE STATIONARY

KALIHAMWE STATIONARY

Nov 28, 2015

MKUU WA WILAYA YA KIGOMA KUKAGUA VYOO NYUMBA KWA NYUMBA ILI KUPAMBANA NA KIPINDUPINDU



KATIKA kuhakikisha ugonjwa wa Kipindupindu mkoani Kigoma unatokomezwa, Serikali ya mkoa imesema itafanya zoezi la ukaguzi wa nyumba kwa nyumba kuhusu uwepo na utumiaji wa vyoo katika Manispaa ya Kigoma Ujiji.

Akizungumza na wananchi wa Kata ya Kibirizi hapo jana, Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Saveri Mwangasame amesema kuwa ukaguzi huo utaambatana na kukagua hari ya usafi katika Manispaa hii.



Mwangasame alisema kuwa, ofisi yake inatarajia kuendesha operation hiyo kuanzia jumatatu 30 ili hatua ziweze kuchukuliwa dhidi ya familia zitakabainika kutokuwa na vyoo na wataanzia katika kata ya Kibirizi ambayo inaelezwa kuwa na wagonjwa wa kipindupindu.

“Sasa hivi Kigoma kuna ugonjwa wa kipindupindu na bado hatujatangaza rasmi kuwa kipindupindu kimekwisha hivyo bado tunaendelea kupambana na ugonjwa huo kwa hatua ya kukagua vyoo kila nyumba” alisema Mwangasame.

Aidha Mwangasame alisema kuwa katika zoezi hilo endapo kuna nyumba itabainika haina choo mmiliki wa nyumba atachukuliwa hatua za sheria sambamba na watu ambao hawatumii vyoo badala yake kwenda kujisaidia ziwani.


“Bado kuna watu wanaoga na kujisaidia ziwani, katika hili hatutakuwa na utani kabisa mana mtu akibainika sheria lazima ichukue mkono wake ili iwe fundisho kwa wengine na katika zoezi la kukagua nyumba hadi nyuma na mimi nitakuwepo ili kuonyesha tumedhamilia kupambana na hari hiyo” alisisitiza Mwangasame.

Hata hivyo wakati Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kigoma ikijiandaa kufanya Oparesheni hiyo, wananchi katika Manispaa hii waliwatupia lawama viongozi wa manispaa hasa sekta ya afya kwa kushindwa kuzungukia maeneo ya mji ili kuhimiza suala la usafi.

Shekhe Jariji Rashid alisema kuwa, utekelezaji wa viongozi wa usafi umelegalega kutokana na maeneo mengi kuzagaa uchafu na akatolea mfano eneo la stand ya daradara ambapo baadhi ya madreva hujisaidia nyuma ya magari yao hivyo kusababisha harufu kuzagaa lakini viongozi wa afya hawalijui hilo kutokana na wao kukaa maofisini kwao.


Nae Issa Kalumanzira alisema kuwa, licha ya kuwa viongozi wa Manispaa wanahimiza usafi ila na wao si wasafi kutokana na Zahanati ya Kibirizi ambacho kimetengwa kwaajiri ya wagonjwa wa kipindupindu ila usafi katika vyoo vya zahanati ile ni vichafu.

“Tungetegemea kuwa zahanati ile ndio ingekuwa safi ili kuzuia kipindupindu kuenea kwa watu wengine ila cha ajabu viongozi hawajari hari mbaya ya uchafu katika vyoo na maeneo mengine na sasahivi wanatwambia watatukagua wakati wao wenyewe hawajikagui” alisema Kalumanzira

Hata hivyo wananchi hao wameitaka Manispaa kuacha kuwatupia lawama wananchi mana hata wao zoezi la uondoaji taka katika madampo yasiyo rasmi kwa  muda mwafaka linaonekana kuwashinda hivyo walekebishe tatizo hilo kwanza mana nalo ni chanzo cha Kipindupindu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Manispaa ya Kigoma Ujiji Boniface Nyambelea amezungumzia suala hilo la uzoaji taka kushindwa kufanyika kwa kiwango kizuri ambapo alisema kuwa changamoto inayosababisha ni kukosekana kwa vitendea kazi vya kutosha kama magari kwani mji mzima unategemea magari mawili tena ya kukodi.