Kigoma Online News

FURNITURE

KALIHAMWE STATIONARY

KALIHAMWE STATIONARY

Jan 29, 2016

WAKIMBIZI 130,041 WAINGIA KIGOMA


Afisa Uhamiaji Mkoa wa Kigoma, Naibu Kamishina  Maurice Kitinusa.

Jumla  ya wakimbizi 130,041 wameingia nchini wakitokea nchi jirani ya Burundi kwa lengo la kutafuta hifadhi baada ya kutokea kwa machafuko nchini kwao mapema mwaka jana 2015.

Akizungumza na blog hili hapo jana, Afisa uhamiaji Mkoa wa Kigoma, Naibu Kamishina Mourice Kitinusa, alisema kuwa idadi hiyo ni kuanzia Aprili mwaka jana ambapo wakimbizi hao hupelekwa katika kambi tatu tofauti kwaajiri ya hifadhi.

Alisema kuwa, Mkoa huu una kambi tatu za wakimbizi ikiwemo kambi ya Nyarugusu iliyoko Wilaya ya Kasulu yenye wakimbizi 86,434, Nduta Wilayani Kibondo yenye wakimbizi 41,572 na kambi mpya ya Mtendeli ambayo ina watu 1596.

“Idadi hiyo ni wale ambao wanaingia moja kwa moja kwenye makambi ila wapo ambao hawapiti katika vituo rasmi mana kunapotokea machafuko mtu hukimbilia popote hivyo wengine huingia  vijijini na kujisalimisha kwa viongozi wa vijiji ili kuomba  hifadhi” alisema Kitinusa.

Kitinusa aliongeza kuwa, wakimbizi waliokuwa wakiomba hifadhi mpaka sasa ni 439 hivyo wanasubiria taratibu  zifanywe na UNHCR ili kuwasafirisha makambini ili kuwapatia hifadhi.

Aidha Kitinusa alisema kuwa, kutokana na wakimbizi wengine kushindwa kupitia katika maeneo yaliyotengwa na serikali na kujikuta wakiingia moja kwa moja vijijini, viongozi wa vijiji wanatakiwa kuwachukua na kuwakabidhi katika ofisi za uhamiaji.

“Kupitia suala hilo sasa viongozi wa vijiji tunawaomba watoe ushirikiano  kwa kuwapokea wakimbizi wanaofika katika maeneo yao na kuwakabidhi katika ofisi za uhamiaji pia kwa wale ambao huwa hawajisalimishi basi wawakamate mana ni makosa kukaa na mkimbizi katika eneo lako.

“Pia kwa wanavijiji nao wanatakiwa kutoa ushirikiano pale wanapokutana na wakimbizi basi watoe taarifa kwa viongozi wao badala ya kuwaacha, ifahamike kuwa kutoa taarifa kuhusu uwepo wa wakimbizi katika maeneo yao si makosa bali makosa ni kukaa na wakimbizi bila kutoa taarifa na watu wanaofanya hivyo wakikamatwa hatua za kisheria huchukuliwa dhidi yao” alisema Kitinusa.

Hata hivyo inadaiwa kuwepo kwa ongezeko kubwa la wakimbizi kutoka nchini Burundi wanaoingia nchini kwa lengo la kuomba hifadhi kutokana  na machafuko ya kisiasa yanayoendelea nchini kwao.