Kigoma Online News

FURNITURE

KALIHAMWE STATIONARY

KALIHAMWE STATIONARY

Dec 16, 2015

MADIWANI UVINZA WATAKIWA KUJIUNGA NA BIMA YA AFYA



MADIWANI wa Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma wametakiwa kujiunga na Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) ili wawe na uhakika wa matibabu pindi wanapougua wao na wategemezi wao.

Akizungumza katika kikao cha kwanza cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo hapo jana, Meneja wa NHIF mkoani  Kigoma, Elias Odhiambo, alisema kuwa, kwa mujibu wa sheria ya mwaka 2009 kufungu cha 3 kila diwani anapaswa kuwa mwanachama wa mfuko huo.


Alisema kuwa, ni wazi kuwa kila mtu ni mgonjwa mtarajiwa na ugonjwa unapokuja hautoi  taarifa hivyo  mtu anaweza kuugua kipindi ambacho hana pesa ila kama ameshakuwa mwanachama wa mfuko huo atapata matibabu kwa kutumia kadi ya uanachama bila kulipa pesa yoyote.

Odhiambo aliongeza kuwa, ni vyema kwa madiwani  hao kujiunga na mfuko huo  ili kuwa na uhakika wa matibabu Pia alisema kuwa kwa watakao hitaji kujiunga  watatakiwa kujaza fomu maalumu kwaajili ya vitambulisho vya matibabu.

''Tutawaleteeni fomu za kujaza kwaajili ya vitambulisho kwa wale madiwani wapya ila wale wazamani mtaleta tu vitambulisho vyenu tuwabadilishie kwakuwa nyie hamna haja ya kujaza fomu tena” alisema Odhiambo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mrisho Gambo alisema kuwa, bado katika Wilaya hiyo  hali ya mwitikio wa wananchi kujiunga na bima ya afya ni ndogo ambapo mpaka sasa kuna asilimia 16 tu ya watu waliojiunga.

“Kwanza madiwani mnatakiwa kuchangamkia fursa kwa kujiunga na mfuko huu na baada ya hapo kuanza kuwahamasisha wananchi nao wajiunge ili itakapofika mwaka 2017 iwe imefika asilimia 80 katika Wilaya hii” alisema Gambo.