Kigoma Online News

FURNITURE

KALIHAMWE STATIONARY

KALIHAMWE STATIONARY

Jul 11, 2015

UMASIKINI UMEKUWA CHANZO CHA KUDUMAZA ELIMU KIGOMA



IMEGUNDULIKA kuwa suala la umasikini  unaowakabili baadhi ya wakazi mkoani Kigoma  umekuwa chanzo cha kudumaza elimu na hivyo kupelekea baadhi ya Wanafunzi kukatisha masomo na kukimbilia mikoani kufanya kazi za kuajiriwa.

Hayo yamesemwa na Mkazi wa Kijiji cha Kiganza, Kata ya Mwandiga katika Wilaya ya Kigoma mkoani hapa, Ashura Kassim alipokuwa anatoa maoni yake kuhusu changamoto ya baadhi ya Wanafunzi kuacha masomo na kukimbilia mijini kwa kisingizio cha kutafuta maisha.

Alisema hali ya maisha kwa baadhi ya Watu ni mbaya kiasi kwamba ni jambo la kawaida kukuta Mwanafunzi anakwenda Shule kusoma bila kuvaa viatu, sare zimechanika na hana uhakika wa kula chakula pindi anaporudi nyumbani baada ya muda wa masomo.

 “Umasikini wa kipato umekuwa chanzo cha Watoto wetu kuacha Shule na kwenda Mjini kufanya kazi za ndani, kuuza maji na kahawa, wengine kukata nyasi za kulisha Ng’ombe na wapo wanaotiimkia mikoani kufanya kazi za ajab ajabu, hiyo yote chanzo chake ni  Wazazi kukosa fedha za kununua  sare za Shule au viatu.” Alisema Kassim

Aliongeza kuwa inapotokea Mwanafunzi anavaa nguo zenye viraka humfanya akose raha shuleni kutokana na utani na maneno ya kejeli anayopata kutoka kwa Wanafunzi wenzake, jambo linalowafanya baadhi kuamua kukatisha masomo na kukimbilia mjini kutafuta kazi licha ya umri mdogo wanaokuwa nao.

“Ipo haja ya Serikali kuhakikisha inajenga mazingira mazuri kwa Wananchi ili waweze kumudu kujiajiri wenyewe na hivyo kupunguza utegemezi katika Familia, kiasi kwamba Watoto wataona fahari kubaki na Familia zao hata kama hali ya kipato haitakuwa nzuri." Alifafanua zaidi.

Aidha Kassim alishauri kuwa  Serikali ijaribu kutengeneza mitaala yenye mwelekeo wa kuwaandaa Wanafunzi kujiajiri baada ya masomo badala ya hali ilivyo sasa ambapo kila muhitimu katika ngazi mbalimbali za masomo anajiandaa kisaikolojia kuajiriwa na Serikali pindi anapomaliza masomo.

Kwa upande wake Sikudhani Amrani, Mkazi wa Kijiji cha Bitale katika Wilaya ya Kigoma mkoani hapa alisema ipo haja ya Serikali kuboresha miundombinu ya elimu mkoani Kigoma ili kuwafanya Watoto kupenda masomo ya kila siku darasani.

“Mazingira mabaya ya Shule zetu yanawafanya baadhi ya Wanafunzi kuacha Shule na kukimbilia mikoani kutafuta maisha, wanakosa mapenzi ya kusoma na hata Walimu wao wanajiona kama Watu wasio na thamani kutokana na hali mbaya ya Shule zao.” Alisema Sikudhani.

Hali ya miundombinu ya Majengo ya Madarasa katika baadhi ya Shule za Msingi mkoani Kigoma sio ya kuridhisha kutokana na uchakavu, lakini pia kuna uhaba wa madawati kiasi cha baadhi ya Wanafunzi kukaa chini kwenye sakafu.